MTAKUWWA YATAKA SHERIA KALI KUTOKOMEZA UKATILI KWA WANAWAKE NA WATOTO
Na. Richard Bagolele-Chato
Wajumbe wa kamati ya Wilaya ya Mkakati wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto wameiomba serikali kutunga sheria ndogo za vijiji kwa lengo la kudhibiti ajira hatarishi za watoto.
Wakiongea kwa nyakati tofauti wakati wa kikao cha robo ya kwanza cha kamati hiyo kilichofanyika leo tarehe 19 Novemba, 2021wajumbe hao wamesema kumekuwa na utumikishwaji wa watoto katika ajira hatarishi katika maeneo mbalimbali ya wilaya kama vile uuzaji wa bidhaa nyakati mchana na usiku pamoja na uchimbaji wa madini lakini jamii imekuwa haitoi taarifa kwa mamlaka husika juu ya utumikishwaji huo.
Mratibu wa shirika la KIVULINI ndugu Eunice Mayengela amesema kutungwa kwa sheria ndogo hizo kutasaidia kutokomeza ukatili dhidi ya watoto katika maeneo mbalimbali ya Wilaya hivyo amesisitiza kamati za MTAKUWWA ngazi za vijiji na kata ziimarishwe.
Kwa upande wake mwakilishi wa mahakama ndugu Tryphone Bashaya amesema kwa mwaka 2021 jumla ya kesi 27 zinazohusiana na ukatili wa wanawake watoto ikiwemo ubakaji, ilawiti,wizi wa watoto, na mashambulio zimefikishwa mahakamani ambapo kati ya hizo kuna kesi ambazo hukumu zake zimetolewa, nyingine bado zinaendelea na uchunguzi.
Mkuu wa idara ya maendeleo ya jamii ndugu Vicent Bushaija akifungua kikao hicho kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji amelishukuru shirika la KIVULINI kwa jitihada zake za kuziwezesha kamati za MTAKUWA kuanzia ngazi za vijiji hadi wilaya zinatekeleza majukumu yake pamoja na kuhakikisha ukatili dhidi ya wanawake na watoto wilayani Chato unatokomezwa.
Kamati ya MTAKUWA ya Wilaya inaundwa na wawakilishi kutoka ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri, jeshi la polisi, magereza, mahakama, madhehebu ya dini, watoto,wazee maarufu, na vikundi vya akina mama.
MKURUGENZI MTENDAJI
Postal Address: 116 CHATO
Telephone: +255282228007
Mobile:
Barua pepe: ded@chatodc.go.tz
Copyright©2016 CDC . All rights reserved.